Heade

WASICHANA WANAOPATA HEDHI MARUFUKU KUVUKA MTO GHANA

Wasichana katika eneo moja nchini Ghana wamepigwa marufuku kuvuka mto mmoja wanapopata hedhi, na pia kuuvuka mto huo Jumanne.
Marufuku hiyo, ambayo inadaiwa kutolewa na miungu wa mto wa eneo hilo imeshutumiwa sana na wanaharakati watetezi wa haki za watoto.
Hii ni kwa sababu wasichana wengi hulazimika kuvuka mto huo kufika shuleni.
Hii ina maana kwamba wasichana wa wilaya ya Denkyira ya Juu Mashariki, katika mkoa wa kati, wanakabiliwa na hatari ya kutopata elimu.
Mataifa mengi Afrika kusini mwa jangwa la Sahara yamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya kuhakikisha wanafunzi wa kike wanasalia shuleni wakati wanapopata hedhi.
Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Sayansi na Elimu, Unesco, linakadiria kwamba asilimia kumi ya wasichana Afrika kusini mwa jangwa la Sahara huwa hawahudhurii masomo shuleni wanapopata hedhi.
Ripoti moja ya Benki ya Dunia inasema wanawake 11.5 milioni nchini Ghana hukosa huduma na vifaa vya usafi.
Balozi wa usafi wakati wa heshi wa Unicef Shamima Muslim Alhassan ameambia BBC Pidgin kwamba amri hiyo kuhusu sehemu ya Mto Ofin inakiuka haki ya wasichana kupata elimu.
"Inaonekana miungu hawa wana nguvu sana, si ni kweli?" alisema.
"Wakati mwingine huwa nafikiri tunafaa kuomba uwajibikaji kiasi kutoka kwa miungu hawa wanaoendelea kuzuia mambo mengi yasifanyike, wawajibishwe kuhusu jinsi wanavyotumia mamlaka haya makubwa ambayo tumewapa."
Waziri wa mkoa wa kati Kwamena Duncan ametoa ishara kwamba atashirikiana na mwenzake wa mkoa wa Ashanti kutafuta suluhu.
Mto wa Ofin ndio mpaka kati ya mikoa ya Ashanti na Kati.
Katika jamii nyingi huwa kuna itikadi nyingi na miiko kuhusu hedhi.
Nchini Madagascar, baadhi ya wanawake hutakiwa kutooga wanapopata hedhi na Nepal wengine hulazimika kulala katika vyumba maalum mbali na familia.

No comments

Powered by Blogger.