Heade

KUNDI LA KIGAIDI LA ISIS LATUMA SALAMU ZA VITISHO KWA RAIS VLADIMIR PUTIN WA URUSI

Kundi la kigaidi la ISIS limetoa vitisho vikali kwa Rais wa Urusi Vladimir Putin kwa kumwambia kuwa atalipa damu za waislamu anaowaua nchini Syria.

Kundi hilo ambalo limeanza kusambaza vipeperushi mitandaoni vyenye maelezo yanayosomeka kuwa “Putin ni mtu usiyekuwa na imani na utalipa damu ya waislamu unaowaua Syria” vimeanza kusambaa mitandaoni kushinikiza Rais Putin kujiengua katika mapambano nchini Syria.

Vipeperushi hivyo ambavyo vinamuonesha mwanaume akiwa ameshika bunduki aina ya AK-47 vimeanza kusambaa kwa kasi katika miji mikubwa nchini Urusi kwenye maeneo yote muhimu ambayo yanamikusanyiko mikubwa ya watu.

Kwa mujibu wa mtandao unaofungamana na kundi hilo wa Wafa Media umeeleza kuwa lengo lao kubwa la ISIS ni kufanya mashambulizi ya kigaidi kwenye michuano ya kombe la dunia.

Vitisho hivyo vinakuja baada ya Rais Putin mwaka jana kutangaza kuisaidia serikali ya Syria inayoongozwa na Rais Bashar Al-Assad katika kupambana na kundi hilo la kigaidi.

Katika hali ya kuimarisha usalama nchini Urusi, tayari serikali imetangaza kuchukua hatua mbalimbali za kiusalama ikiwemo kufungia mtandao wa Telegram ambao umekuwa ukitumika na kundi hilo na makundi mengine ya kihalifu duniani kutokana na usiri wa data zake.

Mwaka jana jeshi la anga la Urusi lilifanya mashambulizi dhidi ya ISIS katika sehemu za kuhifadhia silaha na kituo cha mawasiliano cha kundi hilo viliharibiwa vibaya nchini Syria.

Hii sio mara ya kwanza kwa kundi hilo kumtishia Rais Putin kwani mwaka jana ISIS walitangaza kufanya mashambulizi ya kigaidi kwenye michuano ya Kombe la Dunia linalotarajiwa kuanza kutimua vumbi mwezi June mwaka huu nchini Urusi.

No comments

Powered by Blogger.