Heade

ALIYEBAKWA AKIWA NA MIAKA 70 ATAKA HAKI KUTENDEKA

MWANAMKE mmoja mkazi wa Mlodaa wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma, Monica Tupa (70) amesema amekuwa akizungushwa tangu alipofanyiwa kitendo cha ubakaji Agosti mwaka huu na kuomba kusaidiwa ili haki iweze kutendeka.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa maadhimisho ya Siku 16 za kupinga ukatili dhidi ya wanawake na watoto, alisema Agosti 14, 2017 alibakwa majira ya usiku akiwa nyumbani wake. “Ilipofika asubuhi nikaongozana na mjukuu wangu hadi kwa mkuu wa kitongoji kutoa taarifa, akaniambia nina hela gani ya kuendesha kesi, ikabidi tuondoke kwenda ofisi ya mtendaji tukakuta ofisi imefungwa,” alisema.

Alisema mtendaji hakuwepo kijijini lakini aliporudi alimpa barua ya kwenda polisi kutoa taarifa wakati huo muda ulishakuwa umeshaenda sana. Alisema baadaye mtuhumiwa alikamatwa na kupelekwa polisi.

“Nilipelekwa hospitali ya misheni ya Mvumi na waliponipima walinikuta na dalili zote kuwa nimebakwa,” alisema. Alisema kama serikali inataka kupunguza vitendo hivi ni muhimu kusaidia wananchi wa vijijini wasio na uwezo wanapofanyiwa vitendo vya ukatili. “Nilibakwa nikaenda kutoa taarifa lakini nikawa nazungushwa tu huku viongozi wengine wa kijiji wakinikatisha tamaa kwa kunitolea maneno ya dharau,” alisema.

Kwa mujibu wa mratibu wa maadhimisho hayo Sarah Mwaga, mkoa wa Dodoma ni miongoni mwa mikoa yenye kiwango cha juu cha ukatili kuliko mikoa mingine. Alisema kwa mujibu wa utafiti wa kitaifa wa Tanzania Demographic Health Survey (TDHS) wa mwaka 2010, mwanamke mmoja kati ya watano au asilimia 20 wameshawahi kufanyiwa ukatili wa kindono maishani mwao.

Pia asilimia 10 ya wanawake Tanzania walifanya vitendo vya kujamiiana kwa mara ya kwanza kwa kulazimishwa na si kwa hiari yao. Alisema asilimia 39 ya wanawake wote wameshawahi kufanyiwa ukatili wa kijinsia wa kimwili ikiwemo kipigo, shambulio la mwili au kuumizwa mwilini katika maisha yao.

No comments

Powered by Blogger.