RAIS wa Uganda, Yoweri Museveni amesema, amefikisha umri wa miaka 73 kwa sababu hanywi pombe na hana muda wa kuugua.
Mwanasiasa huyo amezungumzia umri wake, siku chache tu baada ya
kusema kuwa kwa kuwa yeye ni Mkristu na mfuasi wa Yesu Kristu, haogopi
kifo kwa sababu anaamini atafufuka.
Museveni ameandika kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa
twitter kuwa, ukiwa mlevi unakuwa kwenye hatari ya kupata magonjwa,
yakiwemo yanayosababishwa na virusi vinavyosababisha upungufu wa kinga
mwilini (Ukimwi).
“Nimekuwa hapa kwa miaka 30 iliyopita na kwa muda wote huo hamjasikia
kwamba Museveni ni mgonjwa na amelazwa. Sina muda wa kuugua,” aliandika
kiongozi huyo kwenye ukurasa huo. Museveni amekuwa Rais wa Uganda tangu
mwaka 1986.
Kwenye ukurasa huo, Rais Museveni alisema, magonjwa mengi
yangezuilika milele, kama watu wangejihakikishia usafi unaohitajika,
wangepata lishe nzuri, wangelala kwenye vyandarua vyenye dawa ya kuua
mbu, na wangepata kinga.
“Pia watu waache tabia hatarishi na ulevi kwa sababu wanakuwa kwenye
hatari ya kupata magonjwa kama vile Ukimwi,” aliandika Rais Museveni.
Siku chache kabla ya kuandika hayo, Rais Museveni alihudhuria mazoezi ya
wanajeshi ya kupiga risasi katika Kituo cha Mafunzo ya Kijeshi cha
Karama, ambako alitoa ushauri kwa askari kuacha mitindo hatarishi ya
maisha.
“Hongera kwa askari na ushauri wangu kwao ni kwamba wajiepushe na
mitindo hatarishi ya maisha, waepuke umalaya, pombe na rushwa. Maisha
yenu siku zijazo ni mazuri,” aliandika kwenye ukurasa huo wa twitter.
Wakati anazungumza na Wakristu kwenye uwanja wa Akii-Bua mjini Lira,
wakati akizindua uchangiaji wa ukarabati wa Kanisa Kuu la Jimbo la Lira,
Rais Museveni alisema kwa kuwa yeye ni mfuasi wa Yesu Kristu, haogopi
kifo, na atakishinda kwa kufufuka.
Kiongozi huyo alisema ufufuo wa Yesu Kristu, unathitisha kwamba hata
yeye anaweza kufufuka. “Sasa sisi wote ni Wakristu, kwa nini? Kwa sababu
Yesu alikuja, akateswa na alizikwa lakini alifufuka. Alipofufuka
alitupatia tumaini kwamba, sisi pia tutafufuka,” alisema Rais Museveni.
Katika hadhara hiyo, Museveni aliunga mkono kilichoandikwa kwenye
kitabu cha 1 cha Wakorinto 15:26 kwenye Bibila Takatifu kwamba ‘Adui wa
mwisho atakayeangamizwa ni kifo’ “Kama hakuna ufufuko hakuna Ukristu.
Bado sijafa na kufufuka, lakini natumaini kwa sababu mimi ni Mkristu”
alisema.
No comments