Heade

DAGAA ZIWA VICTORIA KULISHA NCHI TANO

WITO umetolewa kwa wafanyabiashara kutoka nchi za Kenya, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Zambia, Malawi na Uganda kujitokeza kununua dagaa waliofurika katika Soko la Samaki Kirumba Mwaloni, jijini Mwanza.

Ziwa Victoria lipo katika nchi tatu za Tanzania, Kenya na Uganda, lakini Tanzania ikiwa na eneo kubwa la ziwa hilo, asilimia 49. Kenya ina asilimia sita na Uganda ina asilimia 45.

“Kwa sasa dagaa na samaki wengine wanapatikana kwa wingi sokoni hapa, hivyo tunawakaribisha wateja wetu wakuu kutoka Kenya, DRC, Zambia, Malawi na hata Uganda kuja kununua bidhaa hizi.

“Wateja wetu wengine wakuu ni kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini ikiwamo Dar es Salaam, Mtwara na Pwani, hao wote tunawakaribisha, dagaa wapo wa kutosha,” alisema Mwenyekiti wa soko hilo, Fikiri Magafu katika mahojiano na gazeti hili jijini hapa, jana.

Kwa mujibu wa Magafu, dagaa na samaki wengine wakiwamo aina ya sangara wanaovuliwa katika Ziwa Victoria wameongezeka sokoni hapo tangu Novemba mwaka huu kutokana na ongezeko la maji ziwani kipindi hiki cha mvua zinazoendelea kunyesha.

Hata hivyo, alielezea kuridhishwa na mahudhurio ya wafanyabiashara kutoka DRC akisema wamejitokeza saba katika kipindi cha wiki mbili na kwamba kila mmoja ameweza kununua magunia kati ya 100 na 1,000 yenye dagaa.

Naye muuzaji wa dagaa katika soko hilo, Johari Juma alitoa wito kwa serikali ya Tanzania kulitangaza soko hilo kimataifa na kupunguza ushuru wa bidhaa hizo ili kuvutia zaidi wanunuzi kutoka nje ya nchi.

Soko la Samaki Kirumba Mwaloni lina uwezo wa kuhifadhi magunia 80,000 yenye dagaa kwa wakati mmoja, achilia mbali samaki wengine, matunda na nafaka mbalimbali. Soko hilo lipo kando ya Ziwa Victoria na lina uwezo wa kuhudumia jumuiya ya wafanyabiashara zaidi ya 2,000 wa samaki kwa wakati mmoja.

No comments

Powered by Blogger.