RAIS wa Rwanda, Paul Kagame ametoa mwito kwa nchi za Afrika,
kuboresha mazingira ya biashara sanjari na kuongeza kasi ya mtangamano
ili zifanikiwe kiuchumi kupitia sekta binafsi.
Kwa mujibu wa kiongozi huyo kutoka moja ya mataifa ya Jumuiya ya
Afrika Mashariki (EAC), katika siku zijazo maendeleo na ukuaji uchumi
barani humo utaitegemea zaidi sekta hiyo, hivyo ni muhimu kumaliza
masharti yasiyo ya lazima na ucheleweshaji usio na umuhimu ili kuwa na
mazingira bora ya biashara.
Mbali ya Rwanda, nchi nyingine za EAC ni Tanzania, Kenya, Uganda,
Burundi na Sudan Kusini. Alitoa changamoto hiyo mwishoni mwa wiki, Sharm
el Sheikh, nchini Misri wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Biashara
Afrika 2017 wenye lengo la kukuza uwekezaji ndani ya nchi za Afrika
sanjari na kuongeza ushirikiano kuvuka mipaka.
Ufunguzi wa mkutano huo wa siku tatu ulihudhuriwa na viongozi kadhaa
akiwemo Rais wa Misri Abdel Fattah Al Sisi, Mwenyekiti wa Umoja wa
Afrika ambaye pia ni Rais wa Guinea, Alpha Conde, Rais wa Ivory Coast,
Alassane Ouattara, Rais wa Somalia, Mohamed Abdullahi Mohamed, na Katibu
Mkuu wa COMESA, Sindiso Ngwenya.
“Bara letu lifanye haraka na lishindane kidunia. Hatuwezi kuendelea
kupoteza fursa kwa sababu ya masharti yasiyo na umuhimu yanayoendana na
ucheleweshaji,” alisema Rais Kagame.
Kwa mujibu wa kiongozi huyo, mazingira ya biashara yanaweza
kuboreshwa zaidi kwa kuongeza kasi ya mtangamano ili kuwa rahisi kwa
nchi hizo kufanya biashara baina yao na kuvutia uwekezaji.
“Ndiyo maana ushirikiano kwenye eneo hili unakuwa jambo la msingi kwa
hali ya baadaye ya Afrika. Kama tunavyoona kwa kusainiwa kwa
makubaliano ya eneo huru la biashara la utatu (TFTA) mwaka 2015 hapa
Sharm El Sheikh unaounganisha COMESA (Soko la Pamoja la Nchi za
Mashariki na Kusini mwa Afrika), Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya
ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika bila kutaja eneo huru kubwa la
biashara la bara likiongozwa na Umoja wa Afrika,” alisema Rais Kagame.
Alisema, mchakato unaoendelea wa mageuzi kwenye Umoja wa Afrika
utaongeza kasi ya utekelezaji wa makubaliano hayo. Katika ufunguzi huo,
Rais Kagame pia alizungumzia umuhimu wa kuongeza upatikanaji wa
teknolojia ya habari na mawasiliano ya kisasa ili kuongeza muingiliano.
Alisema mambo hayo yaachwe kwa vijana hususan wajasiriamali. Kwa
mujibu wa Rais Kagame, uchumi uliofanikiwa ni ule wenye uelewa Awali,
Rais Kagame aliwaeleza wajumbe wa mkutano huo kuwa, rasilimali watu
iliyopo Afrika ina thamani zaidi kuliko madini yote na mafuta yaliyomo
barani humo.
Alisema, vijana wanaweza kuwa injini ya mafanikio Afrika kama
watajengewa mazingira watumie uwezo walionao. Alitoa mfano wa Rwanda
kwamba, nchi hiyo imetengeneza mfumo unaohusisha uelewa, ujuzi, na
taasisi.
Kwa mujibu wa Rais Kagame, jambo la msingi si kuhesabu idadi ya watu
barani Afrika ila kutathmini uwezo wao na kujenga mazingira ili watumie
ipasavyo vipawa vyao. “Bara letu ni maarufu kwa mali asili zake lakini
thamani ya mtaji wa watu tulionao, watu wetu, inazidi mafuta yote na
madini kwenye bara hili,” alisema kiongozi huyo anayejiandaa kuwa
Mwenyekiti wa AU.
Mkutano huo wa pili wa biashara Afrika umehudhuriwa viongozi
mbalimbali Afrika wakiwemo wakuu wa nchi na serikali, na wakuu wa
kampuni na mashirika barani humo. “Rwanda tumetengeneza mfumo wa utatu,
uelewa, ujuzi na taasisi ambako unaona teknolojia ikitumika… hizi
taasisi zinatoa mawazo ambayo yanageuka kuwa biashara au bidhaa.
Tumelifanya hili kwa namna ambayo haisaidii Rwanda tu, lakini pia
taasisi za kimataifa zenye makao Rwanda,” alisema Rais Kagame. Mfumo
mwingine unaotumiwa na Rwanda kutumia vipaji na uwezo wa vijana
unahusisha elimu ya juu ikiwemo ya ufundi na mafunzo na elimu ya ufundi
stadi (TVET) vinavyotoa takribani wahitimu vijana 90,000 kila mwaka.
Rais Kagame ametoa mwito kwa nchi na wajumbe kwenye mkutano huo
kudhamiria kutengeneza fursa kwa vijana wao. “Rwanda inatengeneza mfumo
utakaonufaisha wajasiriamali Waafrika.
Tudhamirie kwa nafasi zetu kutengeneza fursa kwa vijana Waafrika,”
alisema na kutoa mwito kwa vijana kufanya kazi kwa bidii na wasiogope
kujaribu. “Vijana na kila mmoja anayehusika, tunatakiwa kuwa kwenye
ubora wetu, ni jukumu letu, jamii zetu na bara kufanya kazi kwa bidii na
kuendelea kujaribu, tusiache kujaribu…” alisema Rais Kagame.
Wazungumzaji wakuu wengine kwenye mkutano huo ni pamoja na Rais wa
Misri, Al Sisi, mfanyabiashara bilionea wa Nigeria, Tony Elumelu na
mabalozi wajasiriamali vijana, Jean Bosco Nzeyimana, na Mohamed Azab.
No comments