Heade

KENYA YAADHIMISHA MIAKA 54 YA UHURU

Kenya inaadhimisha leo Jumanne Desemba 12 siku kuu ya Jamhuri, siku ambayo nchi hiyo ilijipatia uhuru kutoka kwa Wakoloni Waingereza, miaka 54 iliyopita. Sherehe za maadhimisho ya ya miaka 54 ya uhuru wa Kenya zitafanyika katika uwanja wa Kimataifa wa Michezo wa Moi Kasarani.

Wananchi wa Kenya wameanza kuwasili katika uwanja huo ulioko katika maeneo ya barabara kuu ya Thika, kilomita 10 kutoka katikati mwa mji mkuu Nairobi.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Kenya usalama umeimarishwa na polisi wengi walitumwa katika maeneo mbalimbali ya miji.

Maadhimisho hayo yataongozwa na Rais Uhuru Kenyatta.

Mwishoni juma lililopita muungano wa upinzani NASA ulitishia kumuapisha kiongozi wao Raila Odinga siku hii ya leo kama rais wa watu wa Kenya, lakini Jana Jumatatu muungano huo ulijirudi na kusema shughuli ya kumuapisha kiongozi wao imeahirishwa kwa tarehe nyingine ambayo haikutajwa.

Raila Odinga ambaye anaendelea kupinga kuchaguliwa kwa rais Kenyatta na Stephen Kalonzo Musyoka, walikua wanatarajiwa kuapishwa siku ya Jumanne Desemba 12 kama rais na makamu wa rais mtawalia wa Jamhuri ya Kenya.

Wajumbe kutoka nchi za magharibi na Kanisa wanapendelea mazungumzo kati ya rais Kenyatta na Odinga yafanyike kufuatia wasiwasi kuwa njia iliyochaguliwa na upinzani ilikuwa inalenga kuzusha machafuko.

Siku ya Jumamosi rais Kenyatta alisema hayuko tayari kwa mazungumzo yoyote kuhusu mabadiliko ya uchaguzi.

Vyombo vya usalama vimejiandaa kuhakikisha haviruhusu mkusanyiko wa upinzani leo Jumanne jijini Nairobi wakati rais Uhuru Kenyatta atakuwa akiwaongoza wakenya kuadhimisha siku kuu ya Jamhuri katika uwanja wa Kasarani.

Shinikizo zimekua zikiongezeka kumtaka kiongozi wa muungano wa upinzani nchini Kenya kuachana na mpango wake wa kuapishwa kama rais wa watu siku ya Jumanne Desemba 12.

Odinga alijiondoa kwenye uchaguzi mkuu ambao ulifanyika tarehe 26 mwezi Oktoba ambapo Uhuru Kenyatta aliibuka mshindi.

Uchaguzi huo wa tarehe 26 ulikuwa ni marudio ya uchaguzi mkuu, baada ya mahakama ya juu nchini nchini Kenya kufuta matokeo ya uchaguzi wa Agosti 8 mwaka 2017.

No comments

Powered by Blogger.