Kenya
inaadhimisha leo Jumanne Desemba 12 siku kuu ya Jamhuri, siku ambayo
nchi hiyo ilijipatia uhuru kutoka kwa Wakoloni Waingereza, miaka 54
iliyopita. Sherehe za maadhimisho ya ya miaka 54 ya uhuru wa Kenya
zitafanyika katika uwanja wa Kimataifa wa Michezo wa Moi Kasarani.
Wananchi
wa Kenya wameanza kuwasili katika uwanja huo ulioko katika maeneo ya
barabara kuu ya Thika, kilomita 10 kutoka katikati mwa mji mkuu Nairobi.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Kenya usalama umeimarishwa na polisi wengi walitumwa katika maeneo mbalimbali ya miji.
Maadhimisho hayo yataongozwa na Rais Uhuru Kenyatta.
Mwishoni
juma lililopita muungano wa upinzani NASA ulitishia kumuapisha kiongozi
wao Raila Odinga siku hii ya leo kama rais wa watu wa Kenya, lakini
Jana Jumatatu muungano huo ulijirudi na kusema shughuli ya kumuapisha
kiongozi wao imeahirishwa kwa tarehe nyingine ambayo haikutajwa.
Raila
Odinga ambaye anaendelea kupinga kuchaguliwa kwa rais Kenyatta na
Stephen Kalonzo Musyoka, walikua wanatarajiwa kuapishwa siku ya Jumanne
Desemba 12 kama rais na makamu wa rais mtawalia wa Jamhuri ya Kenya.
Wajumbe
kutoka nchi za magharibi na Kanisa wanapendelea mazungumzo kati ya rais
Kenyatta na Odinga yafanyike kufuatia wasiwasi kuwa njia iliyochaguliwa
na upinzani ilikuwa inalenga kuzusha machafuko.
Siku ya Jumamosi rais Kenyatta alisema hayuko tayari kwa mazungumzo yoyote kuhusu mabadiliko ya uchaguzi.
Vyombo
vya usalama vimejiandaa kuhakikisha haviruhusu mkusanyiko wa upinzani
leo Jumanne jijini Nairobi wakati rais Uhuru Kenyatta atakuwa
akiwaongoza wakenya kuadhimisha siku kuu ya Jamhuri katika uwanja wa
Kasarani.
Shinikizo zimekua zikiongezeka kumtaka kiongozi wa
muungano wa upinzani nchini Kenya kuachana na mpango wake wa kuapishwa
kama rais wa watu siku ya Jumanne Desemba 12.
Odinga alijiondoa kwenye uchaguzi mkuu ambao ulifanyika tarehe 26 mwezi Oktoba ambapo Uhuru Kenyatta aliibuka mshindi.
Uchaguzi
huo wa tarehe 26 ulikuwa ni marudio ya uchaguzi mkuu, baada ya mahakama
ya juu nchini nchini Kenya kufuta matokeo ya uchaguzi wa Agosti 8 mwaka
2017.
No comments