Heade

RAIS KENYATA AMPA MASHARTI MAZITO KIONGOZI WA UPINZANI RAILA ODINGA

Siku chache baada ya Baraza la Magavana nchini Kenya kuunda Kamati ya Watu 10, kuongoza mazungumzo ya usuluhishi ili kumaliza mgogoro wa kisiasa unaoendelea nchini humo, Rais Uhuru Kenyatta amesema yupo tayari kukutana na kuzungumza na Raila Odinga, lakini si kwa mambo ya siasa.

Kenyatta amesema mwishoni mwa wiki kuwa, muda wa siasa umekwisha, na kwamba, Wakenya wanasubiri maendeleo na si mazungumzo yasiyokwisha ya mambo ya siasa. Alitoa msimamo huo katika Shule ya Msingi Kinyona Kaunti ya Muranga wakati wa mazishi ya Susan Chege, ambaye ni mama mzazi wa mwakilishi wa wanawake Muranga, Sabina Chege.

Amesema, yupo tayari kuzungumza kuhusu namna ya kuwaendeleza Wakenya na si vinginevyo, hivyo wapinzani wasubiri awamu nyingine ya siasa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu mwaka 2022 watakapochuana na mgombea urais mtarajiwa wa chama cha Jubilee, Naibu Rais wa sasa, William Ruto.

Odinga, Kiongozi wa Muungano wa Vyama vya Upinzani (NASA), anadai hamtambui Uhuru Kenyatta kuwa ni Rais halali. NASA inaundwa na vyama vya The Orange Democratic Movement (ODM), Wiper Democratic Movement-Kenya (WDM-K), Amani National Congress (ANC) na Forum For the Restoration of Democracy- Kenya (FORD-K).

Viongozi wakuu wa muungano huo ni Raila Odinga, Kalonzo Musyoka, Musalia Mudavadi, na Moses Wetangula. Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), ilimtangaza Kenyatta kuwa ni mshindi wa uchaguzi wa marudio uliofanyika Oktoba 26, aliapishwa Novemba 28 kwenye uwanja wa Kasarani jijini Nairobi.

NASA walitangaza kuwa Odinga angeapishwa siku hiyohiyo kuwa Rais wa watu lakini mpango huo ulisitishwa. Mwanasiasa huyo aliyewahi kuwa Waziri Mkuu, akatangaza angeapishwa leo, lakini pia kambi yake imetangaza kuahirisha hadi hapo itakapotangazwa tena.

Wajumbe wa kamati ya usuluhishi ni Gavana wa Turkana, Josephat Nanok ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza la Magavana hao, Gavana wa Siaya Cornell Rasanga, Gavana wa Makueni Kivutha Kibwana na Gavana wa Kakamega, Wycliffe Oparanya.

Wajumbe wengine ni Gavana wa Bomet Joyce Laboso, Gavana wa Uasin Gishu, Jackson Mandago, Gavana wa Kitui, Charity Ngilu, Gavana wa Nyandarua, Francis Kimemia, Gavana wa Meru, Kiraitu Murungi na Gavana wa Kwale, Salim Mvurya.

Kwenye mkutano wao jijini Nairobi, magavana hao walisema kamati hiyo itafanya kazi ya kuzipatanisha pande zinazopingana na ‘kuiponya’ nchi kutokana na mgawanyiko uliojitokeza wakati wa uchaguzi.

Kati ya Agosti na Oktoba mwaka huu, Kenya imefanya uchaguzi wa Rais mara mbili. Kwanza, Wakenya walipiga kura Agosti 8, mwaka huu na IEBC ilimtangaza Kenyatta mshindi, NASA wakapinga mahakamani, na Septemba Mosi Mahakama ya Juu zaidi ikabatilisha matokeo hayo na kuamuru uchaguzi mwingine ufanyike ndani ya siku 60.

Wakenya walipiga kura tena Oktoba 26, IEBC ikamtangaza Kenyatta mshindi. Odinga alitangaza kujitoa kwenye uchaguzi huo ingawa jina lake lilikuwa miongoni mwa wagombea wanane.

Magavana wanasema umefika wakati kwa viongozi wenye mapenzi mema kutekeleza kwa vitendo azma ya kupunguza joto la kisiasa ili nchi iwe na umoja. “Tunaamini kwamba kuna haja kwa sisi magavana kujitolea kuwa nyenzo ya amani nchini kwa kuzingatia hali ya kisiasa ilivyo sasa.

Kwa nafasi yetu sisi ni viongozi na kwa hiyo tunatoa mwito kwa viongozi wote kuungana na kutafuta njia ya kupooza joto la siasa,” alisema Gavana Nanok. Magavana waliwataka viongozi kuacha ajenda zisizo na tija, na badala yake wazingatie maendeleo ya taifa hilo.

Muda mfupi baada ya kupiga kura kwenye kituo kilichopo katika Shule ya Msingi Mutomo, Jimbo la Gatundu Kusini, Kaunti ya Kiambu Oktoba 26 mwaka huu, Kenyatta alisema, baada ya uchaguzi anaweza kuzungumza na Odinga ili kuondoa mgawanyiko nchini humo.

Mwanasiasa huyo aliyegombea urais kupitia chama cha Jubilee alikiri kuwa, Kenya imegawanyika kwa misingi ya ukabila. “Kama kiongozi unayewajibika lazima umtafute na hilo ndiyo lengo langu,” alisema Kenyatta.

“Kama nchi lazima tupambane na ukabila kwa kuwa hatuwezi kufanikiwa kwenye malengo yetu kama tunaendelea na ukabila,” alisema Kenyatta. Wakati wa kampeni, Kenyatta alisema hakuwa tayari kujadiliana na Odinga na pia alikataa kusuluhishwa na mtu kutoka nje ya nchi hiyo kwa maelezo kuwa nchi hiyo haina mgogoro wa kisiasa.

Siku hiyo hiyo ya uchaguzi Spika wa Bunge la Kenya, Justin Muturi alisema, mamlaka hiyo ipo tayari kusimamia mazungumzo kuwasuluhisha Kenyatta na Odinga. Muturi alimuonya Odinga afanye mambo yake kwa kuzingatia sheria na kwamba, Serikali haitaona vema kujadiliana na NASA ambayo inabadili mwelekeo wake na kuwa kitu kinachoendeshwa kinyume cha sheria.

Alisema, kama NASA wanaamua kuwa wapiganaji wa msituni serikali itapambana nao. Odinga alisema, anaweza kujadiliana na Kenyatta kama majadiliano hayo yatakuwa kwa ajili ya kufanyika kwa uchaguzi mwingine, unaoaminika ndani ya siku 90 (tangu Oktoba 26 mwaka huu).

Alisema wakati akihojiwa na kituo cha television cha CNN cha Marekani kuwa, hata kama Kenyatta akitangazwa mshindi wa uchaguzi uliofanyika Oktoba 26, haitakuwa rahisi kwake kuingoza nchi hiyo.

Alisema, wataipinga Serikali kwa amani, na kwamba, kinaanzishwa kikundi kingine ndani ya Nasa kiitwacho National Resistance Movement. Kwa mujibu wa mwanasiasa huyo, wataipinga serikali kwa amani, si kwa maandamano. Odinga amekataa ushauri wa Wamarekani kumwelekeza cha kufanya.

No comments

Powered by Blogger.