SIKU moja baada ya Rais John Magufuli kurudia kukemea vitendo vya
rushwa, aliyekuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi
(UVCCM), Sadifa Juma Khamis jana alipandishwa kizimbani kwenye Mahakama
ya Mkoa wa Dodoma, akikabiliwa na makosa mawili yanayohusu rushwa.
Sadifa, baadaye alinyimwa dhamana kwa madai ya kuhofia kuingilia
uchaguzi. Mshtakiwa huyo ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Donge,
Zanzibar, alifikishwa Mahakamani hapo majira ya saa 4:45 asubuhi na
maofisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) akiwa
katika gari lenye namba za usajili T994 BEM.
Akisoma kesi hiyo mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo,
Joseph Fovo, Wakili wa serikali kutoka Takukuru, Biswaro Biswaro alisema
katika kesi hiyo ya jinai namba 232 ya mwaka 2017, mshtakiwa huyo
alitenda kosa hilo Desemba 9, mwaka huu akiwa nyumbani kwake maeneo ya
Kata ya Mnadani Manispaa ya Dodoma.
Alisema katika kosa la kwanza, Sadifa anadaiwa kuwa akiwa nyumbani
kwake alitoa rushwa ya vinywaji kwa wajumbe ili wamchague mgombea wa
nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa UVCCM, Rashid Mohamed Rashid.
Biswaro alisema kosa la pili analokabiliwa nalo Sadifa ni kutoa ahadi
ya kuwalipia gharama za usafiri wajumbe hao kutoka Dodoma –Kagera kama
zawadi kwao baada ya kumpigia kura mgombea huyo.
Wakili huyo aliwataja wajumbe hao kuwa ni Kadogo Shaaban, Abdallah
Hamimu, Octavian Andrea, Didas Zimbihile, Tasinta Nyamwiza, John
Lufunga, Mtwawafu Kantangayo, Haleluya Ivody, Deocres Kagunila, Emmanuel
Shitobelo, Happiness Rinyogote, Adolf Andrew, Adinani Musheruzi, Editha
Domician na Hashim Abdallah.
Biswaro alisema mshitakiwa huyo, alitenda makosa hayo kinyume na
Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa namba 11 ya mwaka 2007 Kifungu
cha 15(1)(b) na (2). Alisema upelelezi wa kesi hiyo bado unaendelea na
upande wa Jamhuri unaweka pingamizi la dhamana kwa mshtakiwa.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo, Hakimu Fovo alimhoji mshtakiwa huyo
ambapo alikana kutenda makosa yote mawili. Kukosa dhamana Wakili Biswaro
alisema sababu za kuzuia dhamana ya mshitakiwa huyo kutokana na Mkutano
Mkuu wa Uchaguzi UVCCM ni wa siku mbili mfululizo Desemba 10 na 11,
2017 na matokeo bado hayajatangazwa, hivyo kuna uwezekano wa kuingilia
uchaguzi huo.
“Naomba Mahakama itambue uchaguzi bado unaendelea na mshitakiwa hadi
sasa hajakabidhi uongozi bado ni mwenyekiti,” alisema Aidha, alisema
sababu nyingine ni kuwa mashahidi wengi ni viongozi ambao ni Mwenyekiti
na Makatibu; na endapo akiachiwa kwa dhamana, ana kila aina ya ushawishi
anaweza kuvuruga upelelezi.
Kufuatia maelezo hayo, Wakili wa Utetezi, Godfrey Wasonga alipinga
kuzuiwa kwa dhamana na kudai kuwa ni haki ya mtu kwa mujibu wa Katiba ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Alisema kiapo cha kuzuia dhamana hicho kilichowasilishwa mahakamani,
ambacho kimetolewa na Emma Kuhanga (Kamanda wa Takukuru Dodoma) hakina
mashiko. Alisema Uchaguzi wa UVCCM umeshaisha na mshindi tayari
ameshapatikana na hakuna uchaguzi mwingine wa kuingilia au kama kuna
uchaguzi utafanyika kiapo kingesema.
Alihoji sababu za kupelekwa kesi ambayo haijakamilika upelelezi na
kuzuia dhamana kwa mshtakiwa na kwamba mshtakiwa huyo hataweza kuingilia
uchunguzi kwa sababu walizozitoa. “Mteja wangu ni mbunge ni mtu makini
na anaaminiwa asihukumiwe kwa kuwekwa ndani kwa sababu zisizo na
mashiko,” alisema Wasonga.
Aliomba Mahakama itupilie mbali pingamizi hilo na mshtakiwa apewe
dhamana kwa kuwa hataweza kuingilia uchaguzi na uchaguzi mwingine wa
Umoja huo ni hadi mwaka 2022.
Kufuatia mvutano huo, Hakimu Fovo aliahirisha kesi hiyo hadi desemba
19, mwaka huu na kwamba Mahakama ndipo itatoa maamuzi kuhusu suala hilo
na mshtakiwa ataendelea kuwa rumande
No comments