Heade

MH.RAIS JOHN POMBE MAGUFULI AITAKA BENKI KUU YA TANZANIA (BoT) KUTHIBITI MATUMIZI YA FEDHA ZA KIGENI.


RAIS John Magufuli ameitaka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kudhibiti matumizi ya fedha za kigeni katika biashara na huduma nchini ili kulinda nguvu ya fedha ya Tanzania na kukabiliana na uhalifu wa kifedha.

Pia, ameitaka BoT kuongeza usimamizi wa benki zinazoendesha shughuli zake hapa nchini, ikiwemo kuhakikisha zinajiunga na mfumo wa ukusanyaji mapato kwa njia ya kielektroniki na kufuatilia kwa ukaribu utendaji wake wa kila siku ili ziwe na manufaa kwa nchi. Alitoa maagizo hayo jana wakati akifungua tawi la Benki ya CRDB-LAPF Dodoma na kubainisha kuwa hatua hiyo itasaidia kuimarisha uchumi wa nchi.

“Hivi sasa kuna benki 58 hapa Tanzania, BoT ni lazima mzifuatilie kwa ukaribu benki hizi, na zile zisizofanya vizuri chukueni hatua mara moja, ni bora tubakiwe na benki chache kuliko kuwa na benki nyingi zinazofanya vibaya.

“Pia nataka mdhibiti matumizi ya dola, hivi navyozungumza kuna dola milioni moja zimekamatwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, hakuna maelezo yoyote juu ya kuingia fedha hizo, ni lazima tuwe makini,” alisisitiza Rais Magufuli.

Aliipongeza Benki ya CRDB kwa kuendeshwa kwa ufanisi tangu ilipobinafsishwa kutoka serikalini, ambapo katika kipindi cha miaka 10 imelipa kodi serikalini kiasi cha Sh bilioni 800, imetoa ajira kwa Watanzania 3,200, imetoa gawio serikalini la Sh. bilioni 19.5 mwaka huu na imetoa mikopo yenye thamani ya Sh. trilioni 3.5 ambapo Sh trilioni 1 kati yake zimeelekezwa katika sekta ya viwanda na kilimo.

Kuhusu kupungua kwa kasi ya ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi, Rais Magufuli alisema serikali imechukua hatua mbalimbali zitakazoongeza kasi hiyo, zikiwemo kupunguza kiwango cha kisheria cha sehemu ya amana za benki za biashara, kinachotakiwa kuwekwa Benki Kuu kutoka asilimi 10 hadi 8. Hatua nyingine ni kushusha riba ya Benki Kuu mara mbili kutoka asilimia 16 hadi 9, kutoa mikopo maalumu kwa benki za biashara na Benki Kuu kununua fedha za kigeni kwenye soko la jumla la benki ili kuongeza ukwasi wa shilingi kwenye uchumi.

No comments

Powered by Blogger.