Heade

TANESCO YAZIDI KUIMARISHA HUDUMA

SHIRIKA la Umeme Tanzania (Tanesco), limesema kuanzishwa kwa chanzo kingine cha umeme wa maji cha Stiegler’s Gorge, kutazidi kuifanya nchi iwe na umeme wa uhakika na wa gharama nafuu.

Aidha, serikali imepongezwa kwa kuwa mstari wa mbele kusisitiza utunzaji wa vyanzo vya maji. Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco anayeshughulikia Uzalishaji wa Umeme, Abdallah Ikwasa ametoa kauli hizo kwenye mtambo wa kufua umeme wa Kidatu wilayani Kilombero mkoani Morogoro juzi.

Ikwasa alisema kuanzishwa kwa mradi wa Stiegler’s Gorge, kutasaidia kuboresha upatikanaji wa umeme wa gharama nafuu na rahisi, hivyo kusaidia ukuzaji uchumi. “Kwa mradi huu wa Stiegler’s Gorge kitakuwa chanzo kingine cha umeme wa uhakika na utazidi kuufanya umeme unaozalishwa kwa nguvu ya maji kuendelea kuwa rahisi,” alisema Ikwasa.

Mradi wa umeme wa Stiegler’s Gorge katika maporomoko ya Mto Rufiji, unatarajiwa kutoa megawati 2,100 na tayari zabuni zimefunguliwa na kampuni kadhaa zimeshatuma maombi.

Bosi huyo wa Tanesco alieleza kuwa kwa sasa vituo vya kufua umeme kwa kutumia maji, vinatoa megawati 561 na umeme unaozalishwa nchini umefikia megawati 1,060. Alieleza kuwa katika kiwango hicho, vituo vya Tanesco vinazalisha zaidi ya megawati 1,000 na umeme huo unatosheleza mahitaji ya nchi na kuongeza kuwa katika vituo vya kufua umeme kwa kutumia maji zipo changamoto kadhaa lakini wanaendelea kuzitafutia ufumbuzi.

Aliitaja changamoto kubwa ni uharibifu mkubwa wa vyanzo vya maji, ambako kuna uharibifu wa kingo za mito kutokana na shughuli za kilimo, ambacho pia kinasababisha udongo kuingia mtoni na hivyo kupunguza kina cha mito.

Ikwasa alisema moja ya kitu wanachofanya ni kufuatilia miundombinu ili kuwa na matumizi bora na endelevu ya maji, ili maji yatumike kwa kazi zote mbili za kilimo na kufua umeme.

“Tutaendelea kuhakikisha kuwa maji yanapatikana na kuendelea kutoa huduma kwa wananchi ili umeme wa maji uendelee kubaki kuwa wa bei nafuu,” alisema Ikwasa. Vituo vya Tanesco vya kufua umeme kwa njia ya maji ni Hale na New Pangani Falls vya mkoani Tanga, Nyumba ya Mungu mkoani Kilimanjaro, Mtera cha Dodoma na Kidatu na Kihansi vya mkoani Morogoro.

No comments

Powered by Blogger.