Viongozi wa nchi za Kiislamu wanakutana Istanbul, nchini Uturuki kwa mkutano kuhusu uamuzi wa Marekani
kutambua jerusalem kama mji mkuu wa Israel. Viongozi wao wanakutana kwa
wito wa rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan ambaye ana imani kuwa hatua
kali zitachukuliwa.
Hatua ya
rais Donald Trump ya kutambua mji mtakatifu wa Jerusalem kama mji mkuu
wa nchi ya Kiyahudi wiki iliyopita imesababisha sintofahamu katika nchi
za Kiarabu na kushtumiwa na nchi mbalimbali ulimwenguni, huku maandamano
yakiibuka katika nchi kadhaa za Mashariki ya Kati.
Erdogan,
mtetezi mkuu wa taifa la Wapalestina, alikuwa mmoja wa wakosoaji wa
uamuzi huo wa Donald Trump, akilaani hatua ilio "kinyume na sheria ya
kimataifa". Amesema Jerusalem, mji wa tatu mtakatifu wa Uislamu, " ni
mstari mwekundu kwa Waislamu ambao haupaswi kuingiliwa ".
Erdogan
ambaye ni rais wa Jumuiya ya nchi za Kiislamu (OIC), inayojumuisha nchi
57, ameitisha mkutano wa dharura ambapo ana imani kuwa atajaribu
kuunganisha ulimwengu wa Kiislamu dhidi ya hatua hiyo ya rais Donald
Trump.
Lakini kazi itakua ngumu,wakati ambapo ulimwengu wa
Kiislamu umegawanyika na nchi kadhaa katika kanda ya Mashariki ya Kati,
kama vile Saudi Arabia, zinajaribu kukuza mahusiano mazuri na utawala wa
Trump dhidi ya kuongezeka kwa uhasama na nchi ya Iran.
No comments