Heade

VYETI KIDATO CHA NNE VYA WANAFUNZI 100 VYAYEYUKA

ZAIDI ya wanafunzi 100 waliohitimu kozi ya afya katika Chuo cha Sayansi ya Afya St. Aggrey jijini Mbeya, mwaka 2017, wamekilalamikia chuo hicho kwa kushindwa kuwarejeshea vyeti halisi vya kidato cha nne.

Vyeti hivyo ni vile walivyotakiwa kukusanywa, kwa madai ya kwenda kuhakikiwa Wizara ya Afya. Hayo yamesemwa na Rais mstaafu wa Serikali ya wanafunzi wa chuo hicho, Noeli Mng’ong’o. Alisema hayo alipokuwa akizungumzia adha wanazokumbana nazo, ikiwamo kukosa fursa za ajira serikalini na katika taasisi binafsi kutokana na ukosefu wa vyeti halisi vya kidato cha nne.

Alisema mwaka 2015 wanafunzi 112 walijiunga na chuo hicho kwa kozi ya afya ngazi ya jamii kwa kipindi cha mwaka mmoja. Alisema uongozi wa chuo uliwataka wawasilishe vyeti halisi vya kidato cha nne ili vipelekwe Wizara ya Afya kwa ajili ya uhakiki, kama ni kweli walihitimu au la.

Alisema tangu wakabidhi vyeti hivyo Novemba 2015, wamekuwa wakividai kwa uongozi wa chuo, lakini hadi sasa wamekuwa wakizungushwa na hakuna majibu yoyote. “Mkuu wa Chuo, Dk Rex Mwakipiti anadai wamefuatilia wizarani wameambiwa havipo na wala haijawahi kupokea vyeti halisi kutoka chuo hicho,” alisema Mng’ong’o.

Mkuu huyo wa chuo alipotafutwa kwa njia ya simu, kuzungumzia suala hilo, alidai yupo kwenye kikao na kwamba atafutwe wakati mwingine. Mng’ong’o alisema mkuu huyo aliwaeleza kuwa Wizara ya Afya, inadai hawana hata nyaraka zinazothibitisha kama chuo hicho kiliwahi kuwasilisha vyeti halisi vya kidato cha nne vya wanachuo hao kwa ajili ya uhakiki.

No comments

Powered by Blogger.