Heade

WATOTO LAKI NNE NCHINI DRC WAWEZA KUPOTEZA MAISHA KWA SABABU YA UTAPIAMLO

Umoja wa Mataifa umesema watoto wapatao 400,000 wapo hatarini kufariki dunia ndani ya miezi michache ijayo nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC kutokana na Utapiamlo.

Hadi sasa, Utapiamlo nchini humo umewaathiri watoto laki saba na nusu wenye umri chini ya miaka mitano wengi wao wakiwa hatarini kufariki dunia mapema mwakani endapo hali ya dharura haitachukuliwa kuwanusuru.

Kaimu Mwakilishi wa Shirika la kuhudumia watoto (Unicef) Tajudeen Oyewale, amesema hali hiyo imechangiwa na machafuko ya takribani miezi 18 hali ilyowalazimu watu kutawanyika na kusababisha uzalishaji wa chakula kudorora kutokana na watu kuacha kuzalisha chakula ambapo jimbo la kasai limeathirika kwa kiwango kikubwa.

Aidha, ameongeza kuwa watoto hao wanakabiliwa na magonjwa yanayosababishwa na utapiamlo na ni vigumu kufikiwa na huduma za matibabu na lishe inayofaa ili kuokoa maisha yao.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa machafuko kati ya makundi mbalimbali yanayoipinga serikali nchini DRC yamesababisha maelfu ya watu kupoteza maisha huku wengine milioni 1.4 wameyahama makazi yao kwa lazima kutokana na hali hiyo.

No comments

Powered by Blogger.